Serikali yajizatiti kukuza sekta ya kilimo na kuboresha huduma za Afya

HomeKitaifa

Serikali yajizatiti kukuza sekta ya kilimo na kuboresha huduma za Afya

Katavi, Tanzania – Katika ziara yake mkoani Katavi leo Julai 14,2024 , Rais Samia Suluhu Hassan ametangaza hatua muhimu zinazochukuliwa na serikali yake katika kuboresha sekta ya kilimo na afya nchini. Akihutubia wananchi wa Katavi, Rais Samia ameweka wazi mipango ya serikali ya kukuza kilimo kutoka kilimo cha kujikimu hadi kilimo biashara, na kuongeza bajeti ya kilimo ili kufikia malengo makubwa zaidi.

Rais Samia Suluhu Hassan akizungumza na viongozi, Maafisa wa Jeshi la Polisi pamoja na Wageni mbalimbali mara baada ya kufungua Jengo la Makao Makuu ya Polisi Mkoa wa Katavi tarehe 14 Julai, 2024.

Kukuza Sekta ya Kilimo:

Rais Samia amesema, “Serikali yenu imekusudia kukuza sekta ya kilimo, tunatoka kwenye kilimo tulichokizoea cha kulima na kula, sasa tunakwenda kwenye kilimo biashara.” Kwa mujibu wa Rais, serikali imeongeza bajeti ya kilimo kutoka shilingi bilioni 460 huko nyuma hadi shilingi trilioni 1.25 mwaka huu. Ongezeko hili la bajeti linaonyesha dhamira thabiti ya serikali katika kuhakikisha kuwa sekta ya kilimo inakua na kuwa na mchango mkubwa katika uchumi wa nchi.

Rais Samia Suluhu Hassan Akizindua Vihenga, Ghala la Vyakula na Ofisi ya Wataalamu NFRA, ikiwa ni sehemu ya ziara yake leo tarehe 14 Julai, 2024

Aidha, Rais Samia amefafanua malengo ya serikali ya kufikia uzalishaji wa tani milioni tatu za chakula ifikapo mwaka 2030. “Tumeweza kuongeza bajeti ya kilimo kutoka bilioni 460 huko nyuma na mwaka huu bajeti iliyopitishwa na bunge ni trilioni 1.25. Tunajipanga tuweze kufikia tani milioni tatu tutakapofika mwaka 2030, Tanzania yote tuweze kuhifadhi tani milioni 3,” alisema Rais Samia. Hili ni lengo kubwa ambalo linahitaji jitihada za pamoja kutoka kwa wakulima, vijana, na wadau wote wa kilimo ili kufanikiwa.

Rais Samia pia alisisitiza umuhimu wa kilimo biashara katika kutoa ajira kwa vijana. “Tuna vijana wengine ambapo tunatakiwa kuwatafutia ajira na ajira hizo ni kilimo biashara,” alisema. Serikali inaamini kwamba kupitia kilimo biashara, vijana wengi wataweza kupata ajira na kuchangia katika kukuza uchumi wa taifa.

Kuboresha Huduma za Afya:

Katika hatua nyingine ya kuboresha huduma za afya, Rais Samia alitembelea wodi ya watoto wanaozaliwa kabla ya wakati iliyopo Katavi na kufurahishwa na ubora wa huduma zinazotolewa. “Nimekwenda kuangalia wodi ya watoto wanaozaliwa kabla ya kutimia huduma iliyopo pale ni sawasawa na huduma nilipokwenda kuangalia Dar es Salaam wodi ya watoto ambao hawakutimia. Mashine za kisasa, wataalamu wapo nimekuta muuguzi mzuri sana anawahudumia kwahiyo mambo Katavi ni mazuri mno,” alisema Rais Samia.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Dkt,Samia Suluhu Hassan akiwatazama Watoto waliozaliwa kabla ya Muda (Watoto Njiti) alipotembelea na kukagua Maendeleo ya Ujenzi wa Hospital ya Rufaa Mkoa wa Katavi leo Julai 14,2024.

Rais alihimiza wananchi kuunga mkono huduma za bima ya afya ili kuhakikisha afya ya kila Mtanzania inaimarika na kila mmoja anafaidika. “Niwaombe sana twendeni tukaunge mkono huduma hizi za bima ya afya ili afya ya Mtanzania iweze kuimarika, iweze kusambaa na kila Mtanzania afaidike na afya hii,” aliongeza Rais.

Kupitia hotuba yake, Rais Samia ameonyesha dhamira ya serikali ya kuboresha maisha ya wananchi kupitia sekta ya kilimo na afya, na amewataka wananchi kuunga mkono juhudi hizi kwa manufaa ya taifa zima.

error: Content is protected !!