Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) limewataka wateja wao kulipa madeni ya malipo ya kabla na baada ili kuboresha huduma ya umeme iweze kuwa na ufanisi kwa taifa.
Hayo ameyasema jana Juni 19, 2025 jijini Dar es Salaam, Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano wa Shirika la umeme Tanzania (TANESCO) Irene Gowelle wakati akizungumza na waandishi wa habari akizindua kampeni ya lipa deni ,linda miundombinu tukuhudumie ikiambatana na utoaji wa miundombinu ya umeme katika kuilinda.
“Lengo la kampeni yetu ni makubwa mawili la kwanza ni kuhamasisha ulipaji wa madeni kama unavyofahamu tuna wateja wa aina mbili wa kwanza ni wateja wanaolipa kwanza na wale wanaotumia umeme na kulipa baada sasa tunayo changamoto ya uwepo wa madeni ya wateja wa malipo ya baada kwa maana ya wateja wakubwa na wateja wa kati,”
“Tumeona ni vyema tukitumia fursa hii kuweza kuwakumbusha wateja wetu wote nchi nzima kulipa umeme kwenye bili zao kwa hiari kwa sababu kumekuwa na malimbikizo la madeni,” amesema.
“Kwa sisi kama Shirika madeni hayo yanatupa changamoto kuendesha shughuli zetu kwa hiyo tukaona ni wakati mzuri wa kuweza kuwakumbusha wateja wa malipo ya baada kuweza kulipa bili zao za ankara za umeme”amesema Irene.