Kiongozi wa Kanisa Katoliki duniani, Pope Leo XIV, amepongeza mchango na ushirikiano wa Serikali ya Tanzania kwa kanisa hilo, akisema ni ishara nzuri ya kulinda haki, amani na maridhiano.
Ujumbe huo wa papa ulisomwa na Balozi wake nchini, Angelo Accattino, wakati wa Misa Takatifu ya kumsimika Askofu wa Jimbo jipya la Bariadi, Prosper Lyimo, iliyofanyika wilayani Bariadi mkoani Simiyu Region.
“Ninafurahi na kutambua mchango na ushirikiano mkubwa wa Serikali ya Tanzania kwa Kanisa Katoliki. Ushirikiano huu ni ishara njema ya kutetea haki, amani na maridhiano,” ulisema sehemu ya ujumbe wa papa.
Aidha, Papa Leo XIV alimshukuru Askofu wa Jimbo la Shinyanga, Liberatus Sangu, kwa kukubali kugawa sehemu ya jimbo lake ili kuanzisha Jimbo jipya la Bariadi.
Kuanzishwa kwa jimbo hilo kumefanya idadi ya majimbo ya Kanisa Katoliki nchini kufikia 37.


