Lissu arejea Ubelgiji

HomeKitaifa

Lissu arejea Ubelgiji

Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Tanzania Bara, Tundu Lisu amerejea nchini Ubelgiji kufanya mchakato wa kuhuisha kibali chake cha kuishi nchini humo.

Taarifa kutoka Makamu Mwenyekiti wa chama hicho Zanzibar, Salum Mwalim, zilisema mbali na kuhuisha kibali chake, Lissu aliyeenda nchini humo juzi, amekwenda kwa ajili ya kufanyiwa vipimo zaidi vya afya yake.

Alisema vipimo hivyo ni vya kawaida na vikimalizika kiongozi huyo aliyewakilisha chama hicho katika uchaguzi wa urais wa mwaka 2020 atarudi nchini kuendelea na majukumu yake kama kawaida.

“Ni kweli ameondoka jana (juzi), amekwenda Ubelgiji kwa ajili ya ‘medical checkup’ ya kawaida ambayo ana ratiba zake. Atarudi na sio kwamba amekwenda moja kwa moja, atarudi kuendelea na majukumu yake ya kawaida,” alisema Mwalim ambaye alikuwa Mgombea Mwenza wa urais katika Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2020.

Lissu alirejea nchini kutoka Ubelgiji Januari 25, 2023 baada ya Rais Samia Suluhu Hassan kuondoa zuio la mikutano ya hadhara lililowekwa na Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Rais Dk John Magufuli.

error: Content is protected !!