Viongozi 10 Ngorongoro kutojulikana walipo

HomeKitaifa

Viongozi 10 Ngorongoro kutojulikana walipo

Wakati Serikali ikisema uwekaji mipaka katika pori la Loliondo unaendelea vizuri, Mbunge wa Ngorongoro, Emmanuel Ole Shangai ameendelea kulalamika kutojulikana walipo viongozi 10, akiwamo mwenyekiti wa CCM wilayani humo, Ndirango Senge.

Jana, Mkuu wa Mkoa wa Arusha, John Mongella alisema kazi inaendelea vizuri na kwa amani na hakuna vurugu tofauti na tukio lililotokea mwishoni mwa wiki kulipotokea mgogoro uliosababisha askari polisi mmoja kuuawa kwa kupigwa mshale na kufariki.

“Hakuna mgogoro wowote kwa sasa,” alisema Mongella.

Hata hivyo, mkuu huyo wa mkoa alisisitiza kutokuwa na taarifa za kutojulikana walipo viongozi 10, akiwapo huyo mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Ngorongoro kama zinavyotolewa na mbunge wa Ngorongoro, Shangai.

Wengine wasiojulikana walipo ni madiwani, akiwamo wa Arash, Methew Siloma, Luka Kursas (Oloipiri), Rago Mkeka (Maalon), Moloimet Saingeu (Ololosokwani) na Joel Reson wa Malambo. Pia yumo Simon Nairiamu (Piyaya), Shengena Kille (Olorien Magaiduru), Kijoolu Hakiya na Rebeca Leshoko viti maalum.

Akizungumza na Mwananchi, Shangai alisema wananchi 31 pia wamejeruhiwa. “Naomba kuwe na ushirikishaji katika zoezi hili ili kuondoa migogoro,” alisema.

Wakati Ole Shangai akisema hayo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Justine Masejo hakupatikana ili kuzungumzia kupotea kwa watu hao pamoja na majeruhi waliotajwa na mbunge wao.

Hata hivyo, ofisa mmoja wa polisi ambaye hakutaka jina lake litajwe gazetini alisema taarifa za kukamatwa kuhusiana na mgogoro huo na wale wanaohusishwa na mauaji ya polisi zitatolewa muda si mrefu.

“Japokuwa kamatakamata bado inaendelea kwa sababu wanatajana, ila kamanda atatoa taarifa naomba msubiri, ikiwa tayari tutawapata tu,” alisema ofisa huyo.

source: Mwananchi

error: Content is protected !!