Hatimaye mbivu na mbichi kuhusu nani atapewa ridhaa ya kupeperusha bendera ya Chama Cha Mapinduzi ( CCM) kwa nafasi ya ubunge iwe wa kuchaguliwa au viti maalumu kujulikana Agosti 21 na 23 mwaka huu.
Taarifa ya Amos Makalla Katibu wa Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa CCM iliyotolewa Agosti 17, 2025 imebainisha ratiba ya vikao vya CCM kitaifa vyenye ajenda ya uteuzi wa watia nia hao kwa Tanzania Bara na visiwani Zanzibar.
Kwa mujibu wa Makalla vikao hivyo vitafanyika jijini Dodoma chini ya Mwenyekiti wa chama hicho ambaye pia ni Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan Agosti 21 na 23 mwaka huu.
“Kikao cha Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya CCM Taifa kitafanyika tarehe 21 Agosti 2025, kikifuatiwa na Kikao cha Halmashauri Kuu ya CCM (NEC) Taifa kitakachofanyika tarehe 23 Agosti 2025,” imesema taarifa ya Makalla.
Taaarifa hiyo ya CCM ni miongoni mwa hatua muhimu za maandalizi ya ndani ya chama kuelekea uchaguzi mkuu wa Rais, madiwani na wabunge unaotarajia kufanyika Oktoba 29 mwaka huu.
Siku chache zilizopita CCM ilitangaza rasmi wateule wa nafasi ya udiwani kwa kila kata jukumu lililosimamiwa na Halmashauri Kuu ya Mikoa ya CCM.
View this post on Instagram