Asakwa kwa kumng’ata mama yake masikio

HomeKitaifa

Asakwa kwa kumng’ata mama yake masikio

Jeshi la Polisi Mkoa wa Katavi, linamtafuta Michael Msapi (40), mkazi wa Kirando mkoani Rukwa kwa tuhuma za kumjeruhi kwa kumng’ata masikio yote mawili mama yake mzazi aitwaye Winfrida Athanas (63), mkazi wa Kijiji cha Mchangani, Kata ya Ikola Tarafa ya Karema, Wilaya ya Tanganyika.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Katavi, ACP Ali Makame, akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake jana Januari 27, 2023, amesema chanzo cha tukio hilo ni imani za kishirikina kwa kile kinachodaiwa kuwa mama huyo anawaroga watoto na wajukuu zake.

Naye Ofisa Mtendaji wa Kata ya Ikola, Mwela Mrugwa amesema siku ya tukio mtuhumiwa Michael Msapi, alimvizia mama yake, mzazi wakati akiwa amelala usingizi chumbani mwake na ndipo alipoingia  ndani ya chumba hicho na kumnyofoa masikio yake yote mawili kwa kutumia meno yake na kumsababishia mama huyo maumivu makali.

Baada ya kuwa amefanya ukatili huo kwa mama yake mzazi, mtuhumiwa huyo alitokomea baada ya mama yake kupiga mayowe ya kuomba msaada.

Mrugwa amesema baada ya majirani kusikia mayowe hayo walifika haraka kwenye eneo hilo na kumchukua Winfrida na kisha kumkimbiza haraka kwenye kituo cha afya cha Karema, ambako hadi sasa anaendelea kupatiwa  matibabu.

error: Content is protected !!