Tanzania na Ufaransa zatia saini mikataba sita

HomeKimataifa

Tanzania na Ufaransa zatia saini mikataba sita

Serikali za Tanzania na Ufaransa leo zimetia saini jumla ya mikataba sita ya makubaliano kwa nia ya kuendeleza uhusiano baina ya nchi hizo mbili.

Waziri wa Fedha na Mipango wa Tanzania, Mhe. Mwigulu Nchemba na Mhe. Franck Reister, Waziri wa Biashara wa Ufaransa wametia saini baadhi ya mikataba na makubaliano wakishuhudiwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan.

Miongoni mwa makubaliano hayo ni mkataba wa mkopo wa masharti nafuu wenye thamani ya Euro milioni 178 kwa ajili ya kugharamia mradi wa ujenzi wa barabara wa mabasi yaendayo haraka.

Serikali hizo pia zimesaini mkataba wa mkopo wa masharti nafuu wenye thamani ya Euro milioni 80 ili kuimarisha Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania kufikia malengo ya kutoa mikopo ya muda mfupi na mrefu kwa sekta ya kilimo.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Liberata Mulamula ametia saini mikataba mengine ya ushirikiano kwa niaba ya serikali.

Pia serikali za Tanzania na Ufaransa zimesaini tamko la dhamira ya kushirikiana katika eneo la uchumi wa buluu na usalama wa bahari.

Wakati huo huo, Rais Samia ameyasihi mataifa yote kuheshimu makubaliano na maazimio waliyotia saini, kama wajibu wa kuchukua hatua madhubuti katika kulinda bahari.

Rais Samia aliyasema hayo wakati wa kuhutubia mkutano wa siku tatu ujulikanao kama ‘One Ocean Summit’ mjini Brest, Ufaransa, ulioandaliwa na Rais Emmanuel Macron wa Ufaransa.

 

error: Content is protected !!