7 wasimamishwa kukatika umeme kwa Mkapa

HomeKitaifa

7 wasimamishwa kukatika umeme kwa Mkapa

Serikali imewasimamisha kazi watumishi saba akiwemo Kaimu Meneja wa Uwanja wa Benjamin Mkapa, Salum Mtumbuka kufuatia hitilafu ya kuzimika kwa taa katika uwanja huo iliyojirudia wakati Yanga ikicheza dhidi ya Rivers United kutoka Nigeria.

Mwezi Machi mwaka huu taa hizo zilizimika wakati Taifa Stars ilipowakaribisha Ugandan Cranes ya Uganda katika mchezo wa kufuzu fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON).

Taarifa iliyotolewa na Kitengo cha Mawasiliano, Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo imesema Waziri Pindi Chana amemuelekeza Katibu Mkuu wa Wizara hiyo kuchukua hatua.

“Katibu Mkuu Saidi Yakubu amewasimamisha kazi watumishi wanaohusika na uendeshaji wa uwanja kupisha uchunguzi,” imesema taarifa ya Wizara.

Waliosimamishwa ni Manyori Juma Kapesa (Mhandisi wa Umeme wa Uwanja), Tuswege Nikupala (Afisa Utawala wa Uwanja), Dk. Christina Luambano, Yanuaria Imboru, Gabriel Mwasele na Gordon Nsajigwa Mwangamilo.

Katibu Mkuu Yakubu amemteua Milinde Mahona kukaimu nafasi ya Meneja wa Uwanja wa Benjamin Mkapa kuanzia leo Mei Mosi, 2023.

error: Content is protected !!